WEMA


WEMA.
Josephat S. Hema


Ndugu siku zinaenda,kamwe hazirudi nyuma,
Tazama unayotenda,usijepata lawama,
Ujitahidi kupenda,tena uwe na hekima,
Je hili litakushinda?vipi ni gharama wema?


Wengine walijikuta,mioyo inawauma,
Siku zilipowapita,wakidhani ni gharama,
Kumbe muda ni ukuta,bora ufanye mapema,
Mbona bado una siku?vigumu kutenda wema?

Nyumbani unaanzia,kabla ya mbali kufika,
Jirani anaanzia,kuupata uhakika,
Taratibu husambaa,na kuivuka mipaka,
Wema unapoongea,Dunia yatikisika.

Wengine wanadhania,nguvu nyingi hutumika,
Kwamba utagharamia,jambo jema kufanyika,
La hasha ninakwambia,huko ni mbali kufika,
Japo tabasamu toa,yu mtu afarijika.

Jiamini kwa kidogo,nguvuye huwezi jua,
Hata kama ni kidogo,kuna mtu chamfaa,
Mwanzo huwa ni mdogo,vikubwa vyafuatia,
Siupe wema kisogo,kuna watu waumia.

Upendo ndio kitovu,cha wema kwenye dunia,
Mngekuwa watulivu,kama tungezingatiaa,
Tusingetumia nguvu,migogoro kuamia,
Wema huwa msikivu,hekima anatumia.


Tunaishi kwenye ndoto,kuibadili Dunia,
Wema utakuwa wito,kama tumedhamiria,
Japo ni mengi mapito,wema unavumilia,
Kama  ni kuvuka mto,wema ni yetu mashua.

Sasa iwe changamoto,wema kuupalilia,
Jambo hili sio zito,ni hatua kuamua,
Sio  uamuzi toto,japo hilo natambua,
Kwa pamoja uwe moto,wema kwanza tangulia.


No comments:

Powered by Blogger.